Kujifunza kwa Vitendo kwa Elimu ya Juu kuna manufaa makubwa katika kuongeza ufanisi kwa Taaluma husika

Imeelezwa kuwa kujifunza kwa vitendo kwa wanafunzi wa elimu ya juu kuna manufaa makubwa katika kuongeza ufanisi wa taaluma ambazo wanazisomea.

Kujifunza kwa Vitendo kwa Elimu ya Juu kuna manufaa makubwa katika kuongeza ufanisi kwa Taaluma husika

Hayo yameelezwa na Wanafunzi wa Shahada ya Kwanza wa Mwaka wa Tano kutoka Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi za Afya ya Binadamu katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wakati wakizungumza na  SUA Media kuhusu umuhimu wa mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu.

Miongoni mwa wanafunzi hao ni Clementina Dismasi ambaye ameupongeza Uongozi wa Chuo cha SUA kwa kuweka mazingira mazuri kwa wanafunzi kwa ajili ya kusoma kwa vitendo hasa akiieleza namna ambavyo wao  wananufaika zaidi na masomo hayo hata mara baada ya kumaliza Chuo na kujivunia ujuzi ambao wameupata na wanaendelea kuupata kutoka kwa Wakufunzi chuoni hapo.

“Ni vyema kwa wanajamii kushirikiana na SUA ili kupata elimu juu ya utunzaji wa Wanyama wao pale wanapopata tatizo kama magonjwa lakini pia hata kufuatilia afya ya Wanyama wao kwa kuwa wao kama wataalam wapo kwa lengo la kutoa huduma’’, amesema Clementina

Kwa upande wake Makala Moses amesema kuwa  uwepo wa hospitali ya Wanyama katika Chuo cha SUA kumewasaidia wanafunzi wanaosomea Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi za Afya ya Binadamu katika Chuo hicho kujifunza muundo wa Wanyama  kwa undani zaidi na kufahamu changamoto za  Wanyama na kuzitatua kwa vitendo.

 

Nae Mkufunzi Msaidizi Albert Felix amesema  mafunzo kwa vitendo wanayowapatia wanafunzi yanasaidia kuwajenga kwa nadharia na vitendo na kuwawezesha wanafunzi hao kuwa bora ili watakaporudi kwenye jamii waweze kutatua changamoto mbalimbali zinazohusu Wanyama. 

Share this page