Mhe. Nape Kumaliza Tatizo la Mawasiliano SUA Kampasi ya Mizengo Pinda Kabla ya Mwezi wa Sita Mwaka Huu.

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia Mhe. Nape Moses Nnauye amewahakikishia wanajumuiya ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Kampasi ya Mizengo Pinda na wananchi wote wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe Mkoani Katavi kupata mawasilino ya uhakika wa simu pamoja na redio kabla ya mwezi wa sita mwaka huu.

Mhe. Nape Kumaliza Tatizo la Mawasiliano SUA Kampasi ya Mizengo Pinda Kabla ya Mwezi wa Sita Mwaka Huu.

Waziri wa Habari Mawasiliano na teknolojia Mhe. Nape Moses Nnauye akizungumza na Wanajumuiya ya SUA kampasi ya Mizengo Pinda na baadhi ya Wananchi wa jirani na Kampasi hiyo

Mhe. Nnauye ameyasema hayo Januari 9, 2023 alipotembelea kampasi hiyo wakati akiwa kwenye ziara yake ya kikazi na viongozi wakuu wa mashirika yaliyo chini ya wizara yake kama vile TTCL, TCRA, UCSAF, TBC na mengine kwenye mikoa ya mpakani mwa Tanzania kuangalia usikivu na huduma za mawasiliano zilivyo kwa wananchi wanaoishi maeneo hayo.

Amesema Dunia ya leo mawasiliano ndio kila kitu na huko mbeleni swala la mawasiliano litakuwa kitu kingine kikubwa na kwamba itafika mahali kutokuwa na mawasilino ni sawa na kutokuishi ndo maana wameanza kuzungumza kuwa huduma za mawasiliano ni haki za binadamu kwa kuwa vinakufanya uendelee kuishi.

“Kwenye elimu ndio kabisa maana kwenye kazi za tafiti kama za kwenu hapa SUA usipounganishwa na mawasiliano utashindwa kufanya kazi na kutimiza wajibu wako sawasawa, hapa kwenu mnayo huduma kidogo ya TTCL na nimekuja na Mkurugenzi Mkuu wa TTCL aseme mwenyewe atafanya nini maana maagizo yalitoka kwa Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda lazima yatekelezeke, na Mbunge wa Jimbo hili ambaye ni Naibu Waziri wa Katiba na Sheria akinigomea mambo yangu hayaendi kwa hiyo kwa vyovyote lazima tuondoke na majibu ya namna ya kumaliza tatizo hili na litaisha lini ili nikampe majibu Mhe. Pinda” Ameseza Mhe. Nape.

Aliongeza “Siku moja nilikutana na mzee wangu Waziri Mkuu Mstaafu Mzee Pinda akaniambia kwenye kata ya Kibaoni  sasa kuna Kampasi ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo na imepewa jina lake lakini wanahangaika sana kupata mawasiliano maana mtandao ni wa shida sana na mimi ndio Waziri wa Habari, nikamwambia Mzee nimekusikia ngoja nione nitafanyaje” alieleze Mhe. Nape.

Akitoa majibu ya namna ya kumaliza tatizo hilo Mkurugenzi Mkuu wa TTCL Mhandisi. Peter Ulanga amesema kwa sasa wataboresha huduma ya mtadao wanaotoa kwenye kampasi hiyo lakini wataleta Mkongo wa Taifa kutoka kwenye kituo chao cha Kizi hadi kufika chuoni hapo na kukamilisha mpango huo kabla ya mwezi wa sita mwaka huu.

2 (1)

Mkurugenzi Mkuu wa TTCL Mhandisi Peter Ulanga akitoa ufafanuzi wana namna ya kutatua tatizo hilo la mtadao kwa Chuo na wananchi wa eneo hilo

“Sisi kama Shirika la Mawasiliano nilishakuwa na kikao na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine Prof. Raphael Chibunda kule kampasi Kuu wameshatupatia mpaka eneo la kujenga Community WiFi ambapo tunaweka WiFi mahali na wanafunzi wanaweza kuitumia, hivyo kwa umuhimu wa Kampasi ya Mizengo Pinda na ombi lako Mhe. Waziri ukiruhusu tutafanya hivyo pia na hapa kwenye kampasi hii lakini pia kama uongozi wa Chuo utatupatia eneo hapa tutajenga mnara kwa ajili ya mawasiliano kwa maana ya matumizi ya simu na line za TTCL 2G, 3G na 4G na tukaomba mnara huohuo TIGO nao wafanye co- location” Alieleza Mkurugenzi Mkuu wa TTCL.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) Bi. Justina Mashiba amesema ni jukumu la taasisi yake kupeleka huduma za mawasiliano vijijini maana makampuni ya simu yanaona kuna baadhi ya maeneo ya vijijini hayapati faida kwa hiyo serikali inaongeza ruzuku kidogo ili watanzania wa maeneo hayo wapate huduma za mawasiliano.

3 (1)

Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa mawasiliano kwa wote (UCSAF) Bi. Justina Mashiba akitoa maelezo mbele ya Waziri wa Habari namna mfuko wake utakavyosaidia kupatikana kwa matangazo ya redio na simu katika eneo hilo.

Amesema kuwa wamekuwa wakifanya hivyo kwenye maeneo mengi na katika kata ya kibaoni anayo taarifa kuwa mtandao wa VODACOM unapatikana kwenye eneo hilo lakini kwa speed ya 2G ambayo ni kwa ajili ya kupiga simu tuu lakini haiwezi kutumia simu kubwa na ameongea nao wamemuahidi kabla ya mwezi wa pili watakuwa wamesha kukuza mawasilino na kwenda kwenye 4G ambayo itawawezesha kutumia simu janja zote vizuri na mtadao.

Awali akisoma taarifa fupi ya Kampasi hiyo Rasi wa Ndaki ya Mizengo Pinda Prof. Josiah Katani amesema pamoja na mafanikio makubwa yaliyopatikana toka kunzishwa kwa kampasi hiyo mwaka 2019 pamoja na matarajio makubwa waliyonayo katika kushiriki kwenye kuleta mageuzi kwenye sekta ya Elimu na Kilimo nchini  lakini wanakabiliwa na changamoto mbalimbali hasa ya  mawasiliano.

4 1

Rasi wa Ndaki ya Mizengo Pinda Prof. Josiah Katani akitoa taarifa fupi ya Kampasi hiyo ya Mizengo Pinda.

“Kutopatikana kwa mawasiliano kabisa ya Mtandao wa TIGO na TTCL na hivyo kusababisha kukosa njia mbadala ya mawasiliano, pili chuo kina mnara mdogo wa mawasiliano wa TTCL kwa ajili ya kunasa mawimbi ya internet lakini kasi yake ni ndogo na wakati mwingine mtandao haupatikani kabisa lakini pia mtandao sio wa uhakikwa kupitia mitandao ya simu na hivyo wanafunzi kushindwa kutumia maktaba za kimtandao na vyanzo vingine vya kujipatia machapisho na vitabu na walimu walioko kampasi kuu kushindwa kufundisha kwa masafa kupitia Zoom” Alieleza Prof. Katani.

5 0

Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia Mhe. Nape Moses Nnauye akiwa kwenye picha ya pamoja na Wafanyakazi wa SUA Kampasi ya Mizengo Pinda.

6 0

Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia Mhe. Nape Moses Nnauye akiwa kwenye picha ya pamoja na baaadhi ya viongozi wa Serikali ya wanafunzi SUASO kampasi ya Mizengo Pinda.

7

Rasi wa Ndaki ya Mizengo Pinda Prof. Josiah Katani akikabidhi zawadi Kalenda na Diary za SUA kwa Waziri wa Habari Mawasiliano na Teknolojia Mhe. Nape Moses Mnauye.

IMG 0186

IMG 0188

Wanajumuiya ya SUA Kampasi ya Mizengo Pinda, Wananchi wa Kibaoni,Viongozi mbalimbali wa CCM na Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe wakifuatilia mkutano huo.

Na: Calvin Gwabara – Katavi.

 

Share this page